banner

.

.

Sunday, 2 February 2014

Rose Muhando: Kutoka ombaomba hadi nyota wa muziki wa Injili kimataifa


Maisha uliyoishi zamani hayawezi kukukwamisha kufikia malengo uliyojiwekea. Hakuna mtu ambaye alifikiri leo hii Rose Muhando angeweza kuwa mwanamuziki mkubwa wa nyimbo za Injili anayelipwa fedha nyingi kutokana na muziki wake, hasa kwa wale waliomjua tangu utoto wake.

Lakini mwanamuziki huyo aliyesaini mkataba wa miaka mitano na Kampuni ya Sony Music Africa ya Afrika Kusini alioanza kuutumikia mwaka huu 2014, anasema kuwa maisha yake yalianzia katika hali duni kwani alikuwa akiombaomba baada ya kufukuzwa katika familia yake huko Dumila mkoani Morogoro kwa kosa la kubadili dini.

“Nilikuwa mwimbaji mzuri sana wa kaswida, nilihudhuria kila siku madrasa nikiwa Dumila. Baadaye maisha yangu yalikuwa magumu sana, chanzo cha haya yote ilikuwa ni ugonjwa uliosababisha afya yangu kudhoofu. Kwa wakati huo nilipimwa kila ugonjwa  sikukutwa na tatizo, ndipo siku nilipoamua kwenda katika maombi,” anasema Rose Muhando ambaye sasa anatamba na wimbo Wololo alioutoa chini ya Sony Music Africa.

Anasimulia kuwa baada ya maombi hayo, alipona na hapo ndipo alipoamua rasmi kubadili dini akiwa na umri wa miaka 12.
“Nilipobadili dini, wazazi wangu walichukizwa na uamuzi wangu, waliona ni busara kunifukuza nyumbani, kumbe walizidi kunihatarishia maisha yangu. Niliendelea kutangatanga na baadaye nilipata waume, ambao walinizalisha watoto watatu,” anasimulia na kuongeza:

“Nikiwa na mtoto wa miezi sita niliwahi kufukuzwa na mchungaji mmoja jijini Arusha kwa kuwa tu nilikwenda kumwomba msaada wa fedha kidogo za kurekodi studio. Kitu hicho  kiliniuma sana na sitakisahau katika maisha yangu. Kila nikikaa hukumbuka na kuumia sana.”
Anasema kwamba alifika Arusha kwa ajili ya kurekodi wimbo wake wa kwanza, ambapo kutokana na kutokuwa na fedha aliona ni busara kumwomba msaada mchungaji huyo, lakini ilishindikana.

“Alinifukuza nikiwa na mtoto mchanga aliyekuwa na mgonjwa wa pumu, niliumia sana na hapo ndipo nilipomwambia Mungu nikasema yeye anajua ameniandalia nini kwenye maisha yangu,” anaeleza Rose.

Anasimulia kuwa alianza safari ya kurejea nyumbani, lakini kwa bahati nzuri njiani alikutana na watu wenye asili ya Somalia na kujitambulisha kwao kuwa aliwahi kuwa muumini wa dini ya Kiislamu, nao walimsaidia na kumsafirisha hadi mkoani Morogoro.

Baada ya kufika Morogoro aliendelea na maisha na baadaye kujiunga na kwaya moja mjini Dodoma, wakati huo alikuwa tayari na watoto watatu akiwa pia ameshaokoka.

“Nilianza muziki katika kwaya iliyopo Dodoma, baadaye nikawa mwalimu wa kwaya hiyo ya Dodoma St. Mary’s katika Kanisa la Kianglikana la Chimuli. Niliendelea hivyo mpaka nilipoamua kuanza kutunga nyimbo zangu mwenyewe kwa msaada wa mfuko wa kwaya yetu,” anabainisha na kuongeza:

“Januari mwaka 2005, ndipo nilipoanza kuona uwepo wa Mungu, nilipokea tuzo mbalimbali ikiwamo ya MtunziBora wa nyimbo za Injili, Mwimbaji Bora na Albamu Bora ya Mwaka, zilizotolewa na Tanzania Gospel Music Awards 2004.”

Tupe maoni yako